Fundi wa kuziba Pancha Harson Solomoni 38 amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela baada ya kutiwa hatiani kwa kupatikana na Misokoto 601 ya bangi.Bwana Solomoni ni miongoni mwa washitakiwa wa mwanzo kufungwa kwa sheria hiyo mpya ya udhibiti wa dawa za kulevya iliyosainiwa mei 2015.
Awali sheria ilikuwa inatoa mwanya wa faini kwa mtuhumiwa.Kifungo cha 11(1) cha sheria mpya kinaeleza wazi mtu anayezalisha, kumiliki, kuuza ,kununua au kusafirisha dawa za kulevya ikiwemo Bangi adhabu yake ya chini ni kifungo cha miaka 30 jela.Hukumu hiyo ilitolewa jana na Hakimu Mkazi Mfawidhi Joachim Tiganga baada ya kuridhishwa bila kuacha shaka na ushahidi upande wa Mashitaka.
Wakili wa Serikali Ignas Mwinuka alidai kortini kuwa disemba 1 mwaka 2015 katika maeneo ya Mwika Kimangala Moshi vijijini mshitakiwa alipatikana na kiasi hicho cha bangi pia anadaiwa kuruhusu eneo lake kutumika kuuza Bangi na Gongo.
Akisoma hukumu hiyo Hakimu Tiganga alisema matumizi ya dawa za kulevya yanazidi kuongezeka nchini na kuathiri jamii.
Hivyo mahakama inatoa adhabu hiyo iwe fundisho kwa wengine.
Katika kipindi chote tangu afikishwe kortini kwa mara ya kwanza disemba 1 mwaka jana mshitakiwa alikana mashitaka hadi alipotiwa hatiani na kuhukumiwa jana.